-->

NI SAMORA MOISÉS MACHEL NA KILE KILICHOITWA "KUTOKA RUVUMA MPAKA MAPUTO"

.
Na Comred Mbwana Allyamtu.
 
MSUMBIJI.
Msumbiji (kwa Kireno: Moçambique) ni nchi ya Afrika ya Kusini-Mashariki. Msumbiji iko ufukoni mwa Bahari Hindi ikipakana na Tanzania, Malawi, Zambia,Zimbabwe, Afrika Kusini na Uswazi. Upande wa mashariki kuna kisiwa chaMadagaska ng'ambo ya mlango bahariwa Msumbiji. Jina la nchi limetokana na Kisiwa cha Msumbiji (kwa Kireno: Ilha de Moçambique) kilichokuwa boma na makao makuu ya Ureno kwenye pwani ya Afrika ya Mashariki. Sikukuu ya Taifa ni tarehe 25 Juni, ulipopatikana na uhuru mwaka 1975. Uchumi wake ni GDP ni 14689 milioni US$ kwa mujibu wa takwimu ya World Bank 2016. Lakin pia inashika nafasi ya 167 duniani kiuchumi. Tambarare ya pwani ni sehemu kubwa ya kusini mwa nchi, lakini kwendakaskazini upana wake unapungua. Nyuma ya tambarare nchi inapanda hadi kufika uwiano wa tambarare ya juu ya Afrika ya Kusini. Milima mirefu zaidi inajulikana kama INYANGA yenye mita 2500 juu ya Usawa wa bahari iko katika jimbo la Tete inayopakana na Zimbabwe, Zambia na Malawi.
Mito iko mingi, mkubwa zaidi ukiwa ndio Zambezi, halafu Ruvuma mpakani kwa Tanzania, Save na Limpopo. Ziwa la Nyassa ni sehemu ya mpaka na Malawi. Umbo la eneo la nchi ni refu sana: ni karibu kilomita 2000 kutoka mpaka wa Tanzania upande wa Ruvuma kaskazini hadi Maputo iliyoko karibu na Uswazi na Afrika Kusini. Na Pwani ya Bahari Hindi ina urefu wa km2.470. Miji mikubwa zaidi ni Maputo (wakazi 1.191.613), na wa pili ni Matola (wakazi 543.907) na wa tatu ni Beira (wakazi 530.706).
HISTORIA YAKE.
Wakazi wa kwanza wa Msumbiji huaminiwa kuwa wawindaji wa jamii ya WASANI. Katika karne za kwanza BK wahamiaji Wabantu wenye ujuzi wa kilimo na uhunzi ambao walimeza wakazi wa kwanza inavyothibitishwa na DNA na utafiti uliofanyia mwaka 1990. Haijulikani ni lini ya kwamba wafanyabiashara Waarabu walianza kufika ufukoni na kujenga vituo na miji yao. Lakini utamaduni wa Waswahili ulifika hadi sehemu za mwambao wa Msumbiji toka zama za himaya Mrima yani kilwa Hadi leo aina ya Kiswahilii kinazungumzwa kwenye visiwa vya Kirimba. Mto wa Zambezi ilitumika kama njia ya mawasiliano na biashara kati ya Ufalme wa MweneMtapa (Zimbabwe) na wafanyabiashara wa pwani. Taarifa za kimaandishi zinaanza na kufika kwa Wareno. Mwaka 1498 wakati wa uvamizi wa Vasco da Gama alifika akiwa njiani kuelekea Bara Hindi.
Baadaye Msumbiji ikawa koloni la Wareno hadi mwaka 1975 vita vya ukombozi vya miaka 1964-1974 vilipomalizika kwa ushindi. Hata hivyo vilifuata vita vya wenyewe kwa wenyewe miaka 1977-1992. Kati ya FRELIMO na RENAMO iliyo kuwa ikiongozwa na Alfonso Brakama. sasa tumtazame Baba wa taifa la Msumbiji mkomnist Samora Machel katika mchango wa ukombozi wa taifa la msumbiji kuanzia kuzaliwa mpaka kifo chake chenye utata.
SAMORA MOISÈ MACHEL.
Samora Moisés Machel alizaliwa tarehe 29 Septemba,1933 katika kijiji cha Madragoa (kwa sasa Chilembene), mkoa wa Gaza nchini Msumbiji au Mozambique ambayo kwa wakati woye wa ukuwaji wake alishuhudia utawala wa kikoloni wa Ureno. Ureno iliyokuwa imekita mizizi nchini msumbiji kwa zaidi ya miaka 498 ya utawala wa kikoloni. Dr Machel aliyesomea udakitali wa binadamu Alikuwa Kamanda wa Jeshi la Msumbiji, Mwanamapinduzi, Mjamaa na mwenye msimamo mkali wa Kimarx na Kilenin aliyeiongoza nchi ya Msumbiji tangu uhuru wake mwaka 1975 hadi kifo chake kilichotokea usiku wa tarehe 19 Oktoba 1986 katika eneo la milima la Mbuzini, mpakani mwa Msumbiji, Swaziland na Afrika Kusini na kwa namna moja kifo chake kwa ukaribu kilihusishwa na utawala wa kibaguzi wa Afrika kusini (utawala wa kikaburu) pamoja na njama zilizopangwa na taifa la Ureno mjini Maputo na kuja kumaliziwa mjini Durban tarehe 20/8/1986 miezi miwili kabla ya kifo chake kutokea.
Katika harakati za kupigania uhuru wa Msumbiji kutoka kwa wakoloni wa Kireno, Samora Machel alihudhuria mafunzo ya kijeshi ya kujitolea mjini Dar es Salaam. Mala baada ya kutoka masomoni Ureno alikokwenda kusomea udakitali na baadaye alikuwa ni miongoni mwa wapiganaji wa chama cha FRELIMO waliopelekwa nchini Algeria kwa ajili ya mafunzo zaidi katika mpango maalumu wa mafunzo ulio ratibiwa na Tanzania kwa msaada Mkubwa kutoka kwa mwalimu Nyerere na ile iliyokuwa Nchi zilizo kuwa mstali wa mbele katika ukombozi wa bara la Afrika. Aliporejea Tanzania kutoka Algeria, Samora Machel aliteuliwa kuongoza kambi ya mafunzo ya wapigania uhuru wa FRELIMO iliyokuwa KONGWA mkoani Dodoma. Kambi ya kongwa mjini Dodoma ilikuwa ni miongoni mwa kambi zilizokuwa Tanzania zikiwahifadhi makamanda wa vikosi vya ukombozi msumbiji. Ikumbukwe kwamba Tanzania na Algeria zilikuwa nchi muhimu sana katika ukombozi wa bala la Afrika kwani Algeria ndio iliyo kuwa kituo cha mafunzo ya kijeshi na mafunzo ya mistuni, Mikakati katika mapambano, kutoa siraha na vifaa vya mapambano. Huku Tanzania ikiwa ni kituo cha kuwaifadhi wapiganaji, kuongoza mapambano, kusimamia na Kuratibu shughuli zote za mapambano kwa wanahalakati wa ukombozi.
Baada ya FRELIMO kuanzisha vita vya kudai uhuru wa Msumbiji tarehe 25 Septemba, 1964, chini ya Kachelo wa mikakati bwana Edualdo Mondaline aliyekuwa kiongozi wa mwanzoni wa Kikosi cha chama cha kudai uhuru cha FRELIMO. Samora Machel alitokea kuwa Kamanda mahiri na muhimu sana katika mapambano hayo ambaye jina lake lilivuma kwa kasi mno miongoni mwa Makamanda na wapigania uhuru wa FRELIMO kutokana na umahiri wake katika medani.Na kutokana na umahiri huo, alipanda vyeo kwa haraka ndani ya jeshi la wapigania uhuru wa msituni lililokuwa likijulikana kama FPLM hadi kufikia cheo cha Kamanda wa Jeshi baada ya Kamanda wa Kwanza wa Jeshi hilo, Filipe Samuel Magaia, kufariki mwaka 1966. Na katika uchaguzi wa mwaka 1970, mala baada ya kifo cha aliyekuwa kiongozi wa FRELIMO bwana Edualdo Mondaline kuuwawa na makachero wa kireno mjini Dar es salam nchini Tanzania ndipo Samora Machel alichaguliwa kuwa Rais wa FRELIMO. Kamanda mpya wa Jeshi la Kireno la Msumbiji, Jenerali Kaúlza de Arriaga, alitamba kuwa angewasambaratisha na kuwaangamiza kabisa wapiganaji wa FRELIMO kwa muda wa miezi michache tu lakini hakufua dafu licha ya kuanzisha mashambulizi makali mno katika mpango wake wa "Operation Gordian Knot" mwaka 1970 akielekeza mashambulizi zaidi katika ngome za FRELIMO zilizokuwa Cabo Delgado kaskazini ya mbali ya Msumbiji.
FRELIMO chini ya Samora Machel ilijibu mapigo na kuhimili vishindo hivyo ambapo ilianza mashambulizi kutoka kila upande na kuelekeza nguvu upande wa magharibi mwa nchi katika mkoa wa Tete. Mpaka kufikia mwaka 1974, Wareno walikuwa hoi bin taaban katika uwanja wa mapambano. Baada ya kupigwa vya kutosha, Wareno walikubali kutia saini makubaliano tarehe 7 Septemba, 1974 mjini LUSAKA kwa ajili ya kukipa mamlaka kamili chama cha FRELIMO na tarehe rasmi ya Uhuru wa Msumbiji ikapangwa iwe 25 Juni, 1975. Serikali ya mpito iliundwa ikiwa na Baraza la Mawaziri lililojumuisha FRELIMO na Wareno ikiongozwa na Waziri Mkuu JOACHIM CHISSANO. Samora Machel aliendelea kuongoza akiwa Tanzania hadi aliporejea nyumbani Msumbiji kishujaa katika safari iliyoitwa "KUTOKA RUVUMA MPAKA MAPUTO".
Siku ya tarehe 19 Oktoba, 1986, Rais SAMORA MACHEL alikwenda kuhudhuria mkutano mjini Mbala, Zambia, ulioitishwa kumshinikisha Dikteta MOBUTU SESE SEKO wa Zaire juu ya uungaji wake mkono kwa chama cha upinzani cha Angola cha UNITA. Mkakati wa nchi zilizokuwa Mstari wa Mbele ulikuwa ni kupingana na Mobutu Sese Seko na Hastings Kamuzu Banda katika nia ya kumaliza kabisa uungaji wao mkono kwa UNITA na RENAMO, vyama au makundi ambayo nchi hizo ziliyaona kama wasaidizi au vibaraka wa Afrika Kusini. Japokuwa mamlaka za Zambia zilikuwa zimemwalika Samora Machel kukaa mjini Mbala usiku mzima, yeye alisisitiza kurejea Maputo usiku uleule kwa kuwa asubuhi yake, alikuwa amepanga kuwa na kikao chenye lengo la kufanya mabadiliko katika uongozi jeshini.
Kutokana na umuhimu wa kikao hicho kilichokuwa kimepangwa kifanyike asubuhi yake, Samora Machel alikiuka hata maelekezo ya Wizara ya Usalama kwamba Rais hakupaswa kusafiri usiku. Na kweli Samora Machel aliondoka usiku wa tarehe 19 Oktoba, 1986 kwa ndege kurejea Maputo, lakini kwa bahati mbaya hakuweza kuiona tena Maputo kama alivyokuwa amepanga. Ndege yake ilianguka eneo la milima la Mbuzini mpakani mwa Msumbiji, Swaziland na Afrika Kusini, tena upande wa ndani ya Afrika Kusini; yeye Kamanda Samora Machel na watu wengine 33 walipoteza maisha huku watu 9 waliokuwa wamekaa viti vya nyuma ya ndege wakinusurika. Inaaminiwa kwamba ndege yake ilidunguliwa na utawala wa Kibaguzi wa Afrika Kusini wa wakati huo. Safari ya mwisho ya maisha ya Samora Moisés Machel wa Msumbiji ikawa imeishia hapo. Pamoja na historia hiyo ya samora machel sasa tuitazame Ruvuma na umuhimu wake katika harakati za ukombozi wa Msumbiji.
"KUTOKA RUVUMA MPAKA MAPUTO".
HUWEZI kuzungumzia historia ya Uhuru wa Msumbiji pasipo kutaja mkoa wa Ruvuma mahali ambapo vuguvugu zote za ukombozi kwa sehemu kubwa zilifanyika kuhakikisha Msumbiji inakomboka. Eneo la (Mkenda) lililopo Kijiji cha Nakawale Kata ya Muhukuru mkoani Ruvuma ni sehemu muhimu kabisa katika historia ya msumbiji na ndio maana katika makala hii yangu ya ".........Kutoka Ruvuma mpaka Maputo" ni sehemu muhimu ya kuitmbua Msumbiji lakini pia kujua na kutambua mchango wa Tanzania katika ukombozi wa msumbiji hasa mkoa wa Ruvuma. Eneo hilo lililopo kiasi cha kilometa 124 hivi kutoka Songea mjini kwa kizazi kipya ni eneo ambalo huenda likaonekana halina "umuhimu kabisa" wala umuhimu wowote ule, lakini kwa wazee wanaofuatilia historia za majirani wa Tanzania ni kijiji chenye historia iliyozama katika vichwa. Pengine ni kutokana na ukweli huo kijiji ncha jirani mara tu ukivuka mpaka wa Tanzania na msumbiji kuna hifadhi nzuri inayoelezea mipango ya kwanza ya mashambulio dhidi ya Wareno kutokea mto Ruvuma. Kwa namna yoyote ile eneo hilo ambalo ni kitongoji ni muhimu katika historia ya Msumbiji na hata Tanzania lakini ukiachia mbali maelezo ya wakazi wenye umri mkubwa hakuna jitihada zozote zinazoonekana kufanywa kuhifadhi historia mwanana katika ukuombozi wa Afrika hasa taifa la Msumbiji na Tanzania na hili nimekuwa nikilieleza mara kwa mara katika makala zangu.
Katika kijiji cha Mkenda mkoani Ruvuma ni eneo ambalo wapigania uhuru wa Msumbiji waliokuwa wakiongozwa na Rais wa chama cha Frelimo wakati huo miaka ya 1960 Eduardo Mondrane, walipoanzia safari yao yenye furaha na majonzi papo hapo mkoani Ruvuma, na safari ya kwenda kuanza mapambano ya kumng’oa Mreno. Inaelezwa na wakazi wa eneo hilo kuwa hapo ndipo wapigania uhuru wa Msumbiji na vikosi vya kusaidi kutoka Tanzania katika miaka ya 1968 wakiongozwa na Rais wa chama cha Frelimo Eduardo Mondlane na mkuu wa majeshi Samora MaChel waliweka kambi kabla ya kuingia eneo la Congreso. Ilibidi wafanye kituo hapo kujipanga na kutuma watu wa mwanzo kuangalia mahali ambapo walikuwa watengeneze kambi nyingine ya kujipanga wakati wa kusubiri kuanza kwa mashambulizi kwa lengo la ukombozi.
FRELIMO katika harakati za ukombozi ilijituma na Ilikuwa ni kazi kubwa lakini, viongozi ambao ndio wapiganishaji walikuwa na muda mwingi wa kuchora namna watakavyoendesha vita ya Msumbiji na mahali pa kujihami baada ya mapigano ya mwanzo. Pamoja na kwamba kwa sasa kuna daraja la Mkenda linalounga Tanzania kwa upande wa Songea na Congress kwa upande wa Msumbiji, kijiji cha Mkenda yenyewe imebaki tupu kabisa katika historia kwani siku zinavyoenda, simulizi zinavyozidi kuchakachuliwa eneo hilo linabaki katika roho za waliokumbana na kashikashi ya kwanza ya vita vya Msumbiji na kizazi kipya hakina cha kufanya. Ukivuka Mkenda na kuingia Msumbiji , hali ni tofauti sana.Wao wameweka kumbukumbu zao la tukio la siku ya kwanza baada ya kuvuka mto Ruvuma. Na kuanza safari za kwenda Maputo kwa ukombozi Katika eneo hilo la Congreso zipo mpaka nyumba zilizokuwa zikitumika kulala viongozi mbalimbali pamoja na magogo waliyokuwa wakikalia wakati wa mikutano ya kwanza ya mipango ya vita hivyo vya ukombozi. Mimi nakumbuka nilipo fika Msumbiji kupitia hapo kijijini nilishuhudia upande wa Tanzania kudolola kiuchumi huku upande wa msumbiji kukiwa kumehifadhi historia zake za ukombozi.
Na kumbuka nilipo kutana na Alexandre Jalarne mtunza makumbusho hayo ya Taifa ya Msumbiji katika eneo la Congresso akielezea kwa maringo na kujiamini alisema kuwa viongozi mbalimbali wa ndani na nje ya nchi hiyo wamekuwa wakifika katika makumbusho hayo kwa ajili ya kuangalia kumbukumbu mbalimbali zilizohifadhiwa kiasili. Ikumbukwe kuwa Msumbiji hasa kijiji cha Mkenda mkoani Ruvuma ni muhimu sana kwa ukombozi wake na ndio maana Joaqim Chisano aliitaja Msumbiji kuwa ni muhimili wa ukombozi wa Msumbiji. Pamoja na sisi kuipuuza historia hiyo katika mkoa wetu wa Ruvuma sasa wao watu wa Msumbiji hawa hawapati ulazima wa kuvuka mpaka kuja Tanzania hasa kutokana na kwamba hakuna mahali pa kuona wapi akina Machel walikuwapo kabla ya kuvuka mipaka na kuingia Msumbiji kuanza kazi ya kuikomboa Msumbiji kwa kumkabili Mreno.
Hali ya eneo hilo haijabughudhiwa ukiiangalia kwa makini, kwani hata mtu wa kawaida ukifika hapo unaweza kabisa ‘kunusa’ kwa kutumia akili uwepo wa majemedari hao wa zamani wakati wakipanga fyeko la kwanza kwa Wareno. Katika mazungumzo kuelewa siri ya eneo hilo kubaki bado na harufu ya majemedari hao pamoja na miaka mingi kupita, Jalarne alisema kuwa kinachosaidia eneo hilo kubakia katika hali ya uhalisia ni jinsi wananchi wa nchi hiyo wanavyoheshimu na kuogopa sheria za nchi hiyo ambazo ni kali. ‘’Sheria zetu ni kali sana katika uhifadhi wa mali asili, tena unaweza kujikuta umehukumiwa kunyongwa kama utabainika kukata miti katika hifadhi kama hizi, ndio maana unaona miti inaanguka yenyewe na hakuna hata mtu wa kukata kuni’’ Alisema Jalarne. Aliendelea kusema kuwa Wapigania uhuru wa Msumbiji walifanya mkutano wao wa kwanza Juni 22 hadi 25 mwaka 1962 mkutano wa kujadili jinsi ya kupata uhuru mkutano uliofanyika Jijini Dar es Salaam nchini Tanzania. Na baadae wakaanza mikakati yao mkoani Ruvuma kwa ajili ya ukombozi.
Mtunza makumbusho huyo aliendelea kusema kuwa ilipofika mwaka 1968 wapigania uhuru wa nchi hiyo walifika katika kijiji cha (Mkenda) katika mkoa wa Ruvuma na kuweka kambi kabla ya kuingia mkoa wa Congreso Msumbiji kwa ajili ya kufanya mkutano wake wa pili kwa ajili ya kuanza safari ya kwenda kutafuta Uhuru wao nchini Msumbiji. Na ndio maana makala hii nimeipa jina la *"NI SAMORA MOSÉS MACHEL NA SAFARI YA KUTOKA RUVUMA MPAKA MAPUTO"* Kwa mantiki kuwa mkoa wa Ruvuma ni muhimu sana kwa ukombozi wote wa msumbiji. Ukiangalia kwa undani zaidi utaona kuwa Eneo la kijiji cha Mkenda kilichopo Ruvuma lingeweza kuwekwa kumbukumbu ya kitaifa kutokana na historia hiyo muhimu kabla Msumbiji haijapata uhuru wake mwaka 1975. Na nimekuwa nikisema kuwa Tanzania kama ingeamua kuwekeza katika *"urithi wa vivutio vya kihistoria"* pekee tunge ingiza fedha nyingi sana za kigeni na kuchangia katika pato la Taifa kwani nchi ya Misri pekee huingiza fedha nyingi sana karibu 40% ya pato lote hutegemea utalii wa urithi wa historia.
Pamoja na Ruvuma kubeba historia kubwa ya nchi jirani na kujitolea kwa watanzania kupitia wakazi wake wa kijiji cha Mkenda na maeneo yake ya jirani lakini mpaka leo eneo hili halina hata chembe ya ukubwa wa historia yake katika vichwa vya wapigania uhuru na hata hao alioshiriki katika mapambano hayo. Hata hivyo, historia hiyo ambayo ilistahili kufanyiwa kazi na kuenziwa inakwamba zaidi kutokana na eneo hilo kutoendelezwa kwa namna yeyote . Ukifika eneo hili miundombinu yake ni duni, mawasiliano hakuna jambo linalowalazimu wananchi wa eneo hilo kutumia mtandao wa simu wa nchini msumbiji. Mwalimu Salvius Nindi ni miongoni mwa wakazi wa kitongoji cha Mkenda anasema ni kama vile wako katika kisiwa kutokana na kutokuwa na huduma muhimu kama mawasiliano na miundombinu mibovu hasa ya barabara. Hali hiyo huenda ndiyo inayofanya hata watu kutoka Msumbiji wenye hamu ya kuja kuangalia mwanzo wa harakati hizo kushindwa kufanya hivyo. Kuwepo kwa makumbusho eneo hilo ambayo yanaweza kuungwa na mapambano ya wana Frelimo kumng’oa Mreno kwa kuunganisha na maeneo mengine kama makazi ya Mondlane yaliyopo wilaya ya Temeke, Dar es salaam, kambi za kufunza wapiganaji za Nachingwea huko mkoani Ruvuma. Kwa yamkini kabisa mkoa wa Ruvuma ndipo kitovu cha ukombozi wa Msumbiji.
Kama taifa tulihitaji kuwekeza mkoa wa Ruvuma kwa kuendeleza kumbukumbu ya sisi watanzania kutambua juhudi zetu katika ukombzi wa msumbiji Hali hiyo ingeliwezesha watanzania nao kuuona ushiriki wao katika kumng’oa Mreno. Na kwa kuweka makumbusho na kuboresha miundombinu katika maeneo hayo nchi ingeweza kujipatia pato kubwa la taifa kutokana wananchi wengi wa Msumbiji kufuatilia historia yao ambapo wangelifika Mkenda na maeneo mengine yaliyoungwa katika njia ya mapambano ya uhuru wa Msumbiji. ‘’Kungekuwa na makumbusho ya Taifa hapa serikali ingeweza kupata fedha nyingi, si mnaona mimi nilijenga nyumba ya kulala wageni na sasa najenga nyumba ya kitalii, kama serikali ingewekeza ingepata pato kubwa’’ alisema Mwalimu huyo. Serekali kupitia kwa Mkuu wa mkoa wa Ruvuma imekuwa ikisema kuwa serikali inafanya jitiada za kuboresha miundombinu katika maeneo yote yenye vivutio vya utalii ili kuweza kuwavutia watalii.
Serekali ilikiwa ikisema kuwa tayari serikali imejenga daraja kubwa la Mkenda linalounganisha nchi hizo mbili lengo likiwa ni kurahisha mawasiliano na pia kuunga udugu wa nchi hizi mbili ulioanzia katika mapambano ya kudai uhuru wa Msumbiji. Pamoja na kukiri kwamba taifa limechelewa sana kufikiria kuunganisha makumbusho ya Msumbiji na Mkenda kwa ajili ya majukumu ya kutoa simulizi la kweli la historia ya maeneo hayo katika kudai Uhuru wa Msumbiji, bado masuala hayo yanaweza kufanyiwa kazi na Makumbusho ya taifa na hivyo kuunga makumbusho ya Mkenda na yale ya Congresso. Na hii ndio umuhimu wa Ruvuma katika historia ya ukombozi w Msumbiji na ndio maana tukaiita *"...........Kutoka Ruvuma mpaka Maputo"*.
"Mungu ibariki Afrika, Mungu ibariki Msumbiji, Mungu baliki Tanzania, Mungu baliki fikra za Waafrika".
Ndimi: Comred Mbwana Allyamtu.
© copy rights reseved
®written by Comred Mbwana Allyamtu
•Napatika kwa mawasliano
Comred Mbwana Allyamtu
Kwa Tanzania
+255679555526.
+255765026057.
Kwa Rwanda
+250733153930
+250788214234
Kwa DRC
+243 977 860 824
Email- mbwanaallyamtu990@gmail. Com
Share on Google Plus

About Omari Makoo

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment